You are here > News > Friday News

Last Updated:20.8.2010
ENGLISH | SWAHILI | SPORTS
Wabunge zaidi CCM watimkia upinzani
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimezidi kumeguka, baada ya makada wake sita waliotoswa na Kamati Kuu ya chama hicho kuwania ubunge, akiwamo mbunge wa viti Maalum mkoa wa Kigoma anayemaliza muda wake Sijapata Nkayamba na aliyewahi kuwa mbunge wa CCM kati ya 2000 na 2005 Thomas Nyimbo, kuhamia upinzani.
Makada wengine wa CCM waliotimkia upinzani baada ya kura za maoni ni mbunge wa zamani wa jimbo la Songwe, Paul Edward Mtwina aliyehamia Chadema, Kamanda wa UVCCM Wilaya ya Kigoma Vijijini, Optatus Likwelile na Omari Nkwarulo aliyeshindwa kura za maoni katika jimbo la Kigoma Kaskazini.
Habari zilizolifikia gazeti hili jana zimeeleza kwamba, Thomas Nyimbo ambaye ni mbunge wa zamani wa CCM jimbo la Njombe Magharibi, amechukua fomu za kuwania ubunge katika jimbo hilo kupitia Chadema.
Nyimbo alikuwa mshindi katika kura za maoni ndani ya CCM, lakini jina lake lilikatwa na vikao vya juu vya chama hicho vilivyomalizika mjini Dodoma mwishoni mwa wiki iliyopita na badala yake lumteua aliyekuwa mshindi wa tatu katika mchakato huo Gerson Lwenge.
Katika kura za maoni, Nyimbo aliongoza kwa kupata kura 6,795 akifuatiwa na aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo (2005-2010), Stanley Yono Kevela aliyepata kura 3,434 na Lwege aliambulia kura 2,971.
Akizungumza na Mwananchi jana, Nyimbo alithibitisha kuchukua fomu ya kugombea ubunge kupitia Chadema na kwamba anatarajia kuirejesha leo mapema ili kukiwa na tatizo lolote aweze kulishughulikia.
“Nimechukua fomu ndiyo kupitia Chadema na hii siyo hasira bali ni kutokubaliana kwangu na sera ya CCM kudharau matakwa ya wapigakura na badala yake kutekeleza matakwa ya mtu mmoja,”alisema Nyimbo na kutamba kuwa ana uhakika wa kushinda kwani aliombwa na wananchi kugombea nafasi hiyo ya uwakilishi.
Mkenya afungwa miaka tisa kwa kuuza albino
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi, Mkoa wa Mwanza imemuhukumu raia wa Kenya Nathan Mutei (28) kwenda jela miaka tisa ama kulipa faini ya Sh 80 milioni kutokana na kupatikana na makosa ya kusafirisha albino kutoka nchini Kenya kuja kumuuza kwa kiasi cha Sh 400 milioni.
Mutei alihukumiwa adhabu hiyo na hakimu mkazi Angelous Rumisha baada ya kukiri makosa yake muda mfupi tu alipofikisha mahakamani na kusomewa mashitaka saa 8: 46 mchana wa jana.
Hukumu yake ilisomwa kwa muda wa dakika 18 baada ya maelezo ya wakili wa mashitaka kusomwa na hakimu huyo kupitia ikiwa ni pamoja na kumkabidhi Mutei vielelezo vya maelezo yake ili aweze kuhakikisha maelezo yaliyomo ambayo yanaonyesha kuwa alikiri kosa kama ni yake na kwamba ndiye aliyetia sahihi.
Baada ya Mutei kuhakikisha maelezo yake na sahihi kuwa ndiyo na mahakama ilitulia kwa muda wa dakika 35 huku hakimu akiandika na kisha kuomba maelezo ya wakili wa utetezi na utetezi wa Mutei kisha kuanza kumsomea hukumu.
Make Comments About this Article click here